SOYA ONE LIMITED YAKONGA NYOYO ZA WAUGUZI TARIME MJINI – YACHANGIA MAMILIONI KWENYE HARAMBEE YA UNUNUZI WA GARI LA WAFANYAKAZI WA AFYA
Na Daniel Mussa, Tarime
Katika kuendeleza moyo wa uwajibikaji kwa jamii, kampuni ya SOYA ONE LIMITED, inayojishughulisha na uchimbaji wa madini na yenye makao yake katika Kata ya Kenyamanyori, wilayani Tarime, imetoa mchango mkubwa wa fedha katika harambee ya kuchangia ununuzi wa gari kwa ajili ya wafanyakazi wa afya wa Halmashauri ya Mji Tarime.
Shughuli hiyo ilifanyika katika ukumbi wa BlueSky, ambapo ilihudhuriwa na mamia ya watumishi wa sekta ya afya, viongozi wa serikali, na wadau wa maendeleo. Mkurugenzi wa SOYA ONE LIMITED, Bw. Chacha Soya, alikuwa mgeni rasmi na alikabidhi mchango wa mamilioni ya shilingi kusaidia kutimiza azma ya ununuzi wa gari aina ya Coster, litakalosaidia katika usafiri wa pamoja wa wafanyakazi wa afya kwa shughuli mbalimbali.
"Tumeguswa na dhamira ya watumishi wetu wa afya kutafuta suluhisho la changamoto zao kupitia harambee. Kama SOYA ONE LIMITED, hatukusita kushiriki kwa moyo mmoja kwa sababu tunaamini katika kuijali jamii inayotuzunguka," alisema Bw. Chacha Soya.
Watoa huduma wa afya walipokea mchango huo kwa shukrani na furaha kubwa, wakimtaja Bw. Soya kuwa ni mfano wa kuigwa kwa viongozi wa sekta binafsi katika kushirikiana na jamii.
Mmoja wa wauguzi waliohudhuria hafla hiyo alisema:
Tunaishukuru sana SOYA ONE LIMITED kwa kujitokeza. Ndoto yetu ya kuwa na usafiri wa pamoja imeanza kupata mwanga. Hii ni hatua kubwa mbele kwa ustawi wetu na ufanisi kazini."
Naye mmoja wa madaktari waandamizi alisema:
"Huu ni mfano bora wa ushirikiano. Tunatoa shukrani za dhati kwa SOYA ONE LIMITED na tunakaribisha wadau wengine kuunga mkono juhudi hizi za kijamii."
Kwa kauli mbiu yao ya “Jamii Kwanza”, SOYA ONE LIMITED imeendelea kujipambanua kama mdau namba moja wa maendeleo wilayani Tarime, ikiwa ni pamoja na kusaidia afya, elimu, na mazingira.
Tukio la BlueSky limeacha alama ya matumaini na mshikamano, huku jina la Chacha Soya likizidi kupaa kama kiongozi wa kizalendo anayejali ustawi wa jamii kwa vitendo.
Comments
Post a Comment