MWANZO MPYA FOUNDATION YACHANGIA MILIONI MOJA UJENZI WA MSIKITI BAKWATA TARIME
Tarime, Machi 30 – Taasisi ya Mwanzo Mpya Foundation imeonyesha moyo wa ukarimu kwa kuchangia shilingi milioni moja katika harambee ya ujenzi wa Msikiti wa BAKWATA, Tarime Mjini. Tukio hilo limefanyika leo na kushuhudiwa na viongozi mbalimbali, akiwemo Mkuu wa Wilaya ya Tarime, Meja Edward Gowele.
Akizungumza katika hafla hiyo, mwakilishi wa Mwanzo Mpya Foundation alieleza dhamira ya taasisi hiyo kusaidia miradi ya kijamii ili kuimarisha mshikamano na maendeleo ya wananchi. "Tunatambua umuhimu wa nyumba za ibada katika kuleta amani na maadili mema kwa jamii. Huu ni mwanzo wa ushirikiano wetu na jamii ya Tarime," alisema.
Kwa upande wake, Mkuu wa Wilaya ya Tarime, Meja Gowele, aliipongeza Mwanzo Mpya Foundation kwa mchango wao na kuwataka wadau wengine kujitokeza kusaidia maendeleo ya jamii. "Ujenzi wa msikiti huu ni hatua muhimu kwa waumini wa Kiislamu, na michango kama hii inaonyesha mshikamano wa kitaifa," alisema DC Gowele.
Hafla hiyo ilihudhuriwa na viongozi wa dini, wafanyabiashara, na wananchi waliojitokeza kushiriki katika harambee hiyo. Michango zaidi inaendelea kupokelewa ili kukamilisha ujenzi wa msikiti huo unaotarajiwa kuwa sehemu muhimu ya ibada na malezi ya maadili mema kwa jamii ya Tarime.

Comments
Post a Comment