Martine Marwa Atoa Motisha Kangaliani Sekondari, Kijijini kwa Mbunge Waitara
MKURUGENZI WA TAASISI YA WADAU WA MAENDELEO TARIME ATOA MOTISHA KWA WANAFUNZI WA KANGALIANI SEKONDARI
Tarime, Mara – Mkurugenzi wa Taasisi ya Wadau wa Maendeleo Tarime, Ndugu Martine Marwa, ameendelea kuonesha moyo wa kizalendo kwa jamii ya Tarime kwa kufanya ziara maalum katika shule ya sekondari Kangaliani iliyopo katika kijiji anachotokea Mbunge wa Jimbo la Tarime Vijijini, Mheshimiwa Mwita Waitara.
Katika ziara hiyo, Ndugu Marwa alikabidhi rasmi vifaa vya TEHAMA kwa ajili ya kusaidia kuinua kiwango cha elimu katika shule hiyo, baada ya shule hiyo kushika nafasi ya mwisho katika matokeo ya mitihani ya mwisho wa mwaka 2024 katika ngazi ya wilaya na mkoa.
Vifaa vilivyokabidhiwa ni pamoja na kompyuta, printer na vifaa vingine vinavyotarajiwa kuongeza ufanisi katika ufundishaji na ujifunzaji wa masomo mbalimbali, hasa masomo ya sayansi na TEHAMA.
"Tumekuja hapa sio kulaumu bali kuonesha upendo kwa watoto wetu na kutoa msukumo mpya wa matumaini. Tunaamini kuwa kwa vifaa hivi na hamasa hii, Kangaliani itaamka na kufanya vizuri zaidi mwaka huu," alisema Marwa wakati wa hafla ya makabidhiano.
Wananchi, wazazi, walimu na wanafunzi walifurika kushuhudia tukio hilo huku wakionesha shukrani kwa msaada huo muhimu. Walimu wa shule hiyo walieleza kuwa changamoto kubwa imekuwa ukosefu wa vifaa vya kisasa vya kujifunzia, hivyo msaada huo umefika wakati muafaka.
Mwalimu Mkuu wa shule hiyo aliahidi kuwa uongozi wa shule utahakikisha vifaa hivyo vinatumika kwa malengo yaliyokusudiwa na kuwa kichocheo cha kuleta matokeo bora.
[PICHA: Mkurugenzi Martine Marwa (kulia) akiwa na wananchi na viongozi wa shule ya Kangaliani wakati wa hafla ya makabidhiano ya vifaa vya TEHAMA.]
Kwa upande wake, Marwa alitoa wito kwa wadau wengine wa maendeleo ndani na nje ya Tarime kuungana na taasisi yake katika juhudi za kuinua elimu vijijini. Alisisitiza kuwa maendeleo ya jamii yanaanza na uwekezaji katika elimu ya watoto.
Taasisi ya Wadau wa Maendeleo Tarime imejipambanua kama miongoni mwa mashirika yanayogusa maisha ya watu moja kwa moja, ikiwa na kaulimbiu ya kuinua sekta muhimu kama elimu, afya na mazingira kwa vitendo.


Comments
Post a Comment