RAYMOND JOHN OLE MATINDA ATETA NA KAMATI TENDAJI YA JUMUIYA YA WAZAZI CCM TARIME
Ajadili Mpango wa Kujenga Nyumba ya Katibu wa Jumuiya
TARIME, Aprili 30, 2025 — Katibu wa Jumuiya ya Wazazi wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) Wilaya ya Tarime, Ndugu Raymond John Ole Matinda, amekutana na Kamati Tendaji ya jumuiya hiyo kwa kikao maalum kilicholenga kujadili mpango wa kujenga nyumba ya Katibu wa Jumuiya hiyo.
Akizungumza na MBC MEDIA mara baada ya kikao hicho, Raymond amesema kuwa lengo kuu la kikao lilikuwa ni kuweka msingi wa mpango huo muhimu, ambao una dhamira ya kuboresha mazingira ya kazi kwa kiongozi mkuu wa jumuiya hiyo wilayani Tarime.
"Tulikaa kikao cha Kamati Tendaji ambapo tulijadili kwa kina suala la ujenzi wa nyumba ya Katibu wa Jumuiya. Hili ni jambo la msingi katika kuimarisha utendaji kazi wa jumuiya yetu," alisema Raymond.
Alibainisha kuwa hatua hiyo ni mwanzo wa mchakato wa muda mrefu wa kuhakikisha jumuiya ya wazazi inakuwa na miundombinu bora inayowezesha viongozi wake kutekeleza majukumu yao kwa ufanisi.
"Tumeamua kuanza kwa kuweka maono na mwelekeo sahihi. Tutazidi kushirikiana na wanajumuiya na wadau wengine kuhakikisha tunalifikisha lengo hili mahali stahiki," aliongeza Raymond.
Raymond ameendelea kuhimiza mshikamano, nidhamu na moyo wa kujitolea miongoni mwa wanachama ili kuhakikisha ndoto hiyo inatimia kwa manufaa ya jumuiya na chama kwa ujumla.



Comments
Post a Comment